b..

B1

Wynem

animation

Sunday, April 8, 2012

BASATA YATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI NA MASIKITIKO JUU YA KIFO CHA STEVEN CHARLES KANUMBA


PRESS RELEASE
MASIKITIKIO JUU YA KIFO CHA MSANII STEVEN CHARLES KANUMBA
Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limepokea kwa masikitiko na majonzi makubwa taarifa ya kifo cha Msanii wa filamu Steven Charles Kanumba kilichotokea usiku wa kuamkia leo Jumamosi ya Tarehe 07/04/2012 baada ya kuanguka ghafla akiwa nyumbani kwake Sinza Vatican jijini Dar es Salaam.
BASATA inaungana na familia za wafiwa na wasanii wote nchini kwa maombolezo  ya msiba huu mkubwa na wa kihistoria.  Kufiwa na msanii huyu mahili kwenye tasnia ya filamu ni pengo kubwa kwa familia, Sekta ya sanaa na Taifa kwa ujumla kutokana na ukweli kuwa, aliweza kuutangaza utamaduni na sanaa yetu nje ya mipaka.
Kanumba atakumbukwa kwa moyo wake wa kujituma na kuthamini kazi ya Sanaa toka akiwa Kundi la Maigizo la Kaole ambapo moyo wake huo ulimfanya awe miongoni mwa wasanii walioleta mageuzi kwenye tasnia ya filamu kwa kuifanya kuanza kupendwa na wadau wengi zaidi.
Aidha, atakumbukwa kwa juhudi zake za kuinua vipaji vichanga katika tasnia ya filamu ambapo mara kadhaa katika kazi alizoziandaa alishirikisha wasanii wachanga ambao BASATA inaamini watakuja kuwa hazina kubwa kwa taifa letu.
BASATA linatoa pole kwa familia ya marehemu na Wasanii wote katika kipindi hiki kigumu. Ni vema wasanii wote tukatumia kipindi hiki kutathimini kwa pamoja michango yetu katika kukuza sekta ya Sanaa ikiwa ni pamoja na kuimarisha umoja wetu lakini pia tukiyaenzi yale yote mema yaliyofanywa na Steven Charles Kanumba.
Mungu ailaze roho ya Marehemu Steven Charles Kanumba mahali pema peponi. AMEN
Sanaa ni Kazi Kwa Pamoja Tuikuze na Kuithamini.
Ghonche Materego
KATIBU MTENDAJI, BASATA

No comments:

Post a Comment