Msanii G Nako kutoka Kundi la muziki wa kizazi kipya la Weusi akiimba sambamba na msanii mchanga ambaye hakufahamika mara moja kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA mapema wiki hii.
--------xxxxxxxxxxxx----------
Na Mwandishi Wetu
Baadhi ya
wasanii nchini wameiomba Serikali kupitia Wizara ya Fedha kufikiria kupunguza au
kufuta kabisa ushuru wa forodha unaotozwa kwenye vifaa vya muziki wanavyoagiza
kutoka nje ili kukuza Sanaa na kusaidia mamilioni ya vijana ambao wamejiajiri
kupitia sekta hiyo.
Akizungumza
kwa niaba ya wasanii mapema wiki hii kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa
la Taifa (BASATA) mmoja wa wasanii anayeunda kundi la muziki wa kizazi kipya la
Weusi Nick wa Pili alisema kwamba, kwa sasa sekta hiyo ni kimbilio la ajira kwa
vijana wengi kwa hiyo Serikali haina budi kupunguza kodi kwa zana mbalimbali
zinazotumiwa na wasanii ili kurahisisha uzalishaji, kukuza tija na uchumi.
“Wasanii wengi
kwa sasa wanakwenda kufanya video na kutengeneza muziki nje ya nchi. Hii
inatokana na teknolojia yetu kuwa chini ya wenzetu. Naamini Serikali ikipunguza
kodi katika vifaa hivi na kuwawezesha wataalam tulionao basi nchi zote jirani
zitakimbilia kwetu” alisema Nick
Aliongeza
kwamba vipaji vya wasanii vipo vingi lakini kutokana na uzalishaji duni wa kazi
za muziki na hata filamu wasanii wamejikuta wakishindwa kushindana ipasavyo nje
ya nchi na mara nyingi kutumia gharama kubwa katika kufuata teknolojia hizo za
juu nchi za nje na hivyo kuikosesha serikali mapato.
“Wasanii
wanakwenda kulipa zaidi ya milioni arobaini kwa video moja tu nje ya nchi, hizi fedha zinakwenda kukuza uchumi wa nchi zingine. Naamini kama Serikali ikijenga
mazingira mazuri ya kiteknolojia na zaidi kushusha gharama hizi basi nchi yetu
itafaidika zaidi na Sanaa” alizidi kusisitiza Nick.
Kwa upande
wake Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mitaji na Misaada kwa wasanii kutoka BASATA Bi.
Elineca Ndowo alisema kwamba sekta ya Sanaa nchini inazidi kukua na hivyo
lazima wasanii nao wafikirie kufanya kazi kisasa na kwa kufuata taratibu zote
ili kuipa serikali uhakika katika kupanga kulingana na hali halisi.
“Sekta ya
Sanaa inakua, lazima tuisaidie Serikali kuipa takwimu sahihi na moja ya njia ya
kuhakikisha hili ni kwa wasanii kujisajili, kusajili kazi zao na kuhakikisha
taarifa sahihi na kwa wakati zinapatikana. Hili litarahisisha upangaji wa
mipango” alisema Bi. Ndowo.
Jukwaa
la Sanaa la BASATA ni programu ambayo hufanyika kwa mwezi mara mbili siku ya
Jumatatu na hutumika kama jamvi la kuwaelimisha wasanii na kuwakutanisha kwa
pamoja katika kubadilishana uzoefu na mawazo kuhusu masuala mbalimbali yahusuyo
sekta yao.
Msanii anayechipukia kwenye tasnia ya filamu kutoka taasisi ya mafunzo ya TAMAP akiwauliza maswali mbalimbali wasanii wa kundi la Weusi kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA mapema wiki hii.
Msanii wa muziki wa kizazi kipya kutoka Kundi la Weusi Nick wa Pili (Kushoto) akisisitiza jambo wakati akiongea na wadau wa Sanaa (hawako pichani) kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa inayofanyika kwa mwezi mara mbili siku ya Jumatatu makao makuu ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam. Wengine kushoto kwake ni wasanii wanaounda kundi hilo John Simon aka Joh Makini na G Nako na Afisa kutoka BASATA Bi. Elineca Ndowo
Sehemu ya wadau wa Sanaa waliohudhuria programu hiyo ya Jukwaa la Sanaa ya BASATA.
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mitaji na Misaada kwa wasanii kutoka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Bi. Elineca Ndowo (Kulia) akiongea na wadau wa Sanaa (hawako pichani) kuhusu masuala mbalimbali kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa ambayo huandaliwa kwa mwezi mara mbili ziku ya Jumatatu na Baraza hilo. Wengine katika picha kulia kwake ni Wasanii G Nako na John Simon maarufu kama Joh Makini wanaounda kundi la muziki wa kizazi kipya la Weusi.