b..

B1

Wynem

animation

Sunday, July 15, 2012

KAULI ZAMPONZA TUNDU LISU

Na Mwandishi Wetu
MNADHIMU wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu ameingia matatani kutokana na kauli yake kwamba Rais Jakaya Kikwete amekuwa akiteua majaji wa Mahakama Kuu wasiopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Kutokana na kauli hiyo aliyoitoa wakati akiwasilisha maoni ya kambi yake, kuhusu hotuba ya makadirio ya matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria, Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema) atajadiliwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.
Wakati akisoma hotuba yake, mbunge hiyo alisema majaji wanaoteuliwa na Rais hawafanyiwi ‘vetting’ (uchunguzi) na tume hiyo kuona kama uwezo na ujuzi wao unafaa kukabidhiwa madaraka ya ujaji.Mwenyekiti wa Bunge, Jenista Mhagama ndiye aliyeamuru suala la Lissu kupelekwa katika kamati hiyo baada ya mbunge huyo kukataa kufuta kauli yake ambayo kwa mtazamo wa Serikali iliwadhalilisha majaji.Hata hivyo, jana alipotakiwa kueleza kama ana taarifa rasmi za kuitwa kwenye kamati hiyo Lissu alisema:
 “Sijaitwa, lakini nina taarifa kuwa naweza kuitwa.’’Alisema, hata wakimwita hatakuwa na jambo lolote la kuzungumza kwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge aliyeongoza kikao hicho juzi (Jenista Mhagama), alikosea kwa kuwa ndiye aliyepaswa kumpa adhabu.Mbunge huyo alisema  juzi aligoma kufuta kauli yake kama alivyotakiwa na Mwenyekiti kwani aliamini kuwa hata Mwanasheria Mkuu alikuwa amekosea.Alibainisha kuwa endapo ataitwa katika kamati hiyo, atahoji kama waliomwita wamegeuka kuwa wenyeviti wa Bunge na kama si hivyo, anaamini watakosa neno la kumhoji.Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema kwa nyakati tofauti wakati wakijibu hoja za wabunge juzi jioni walisema: “Lissu aliwakashifu majaji bungeni, hivyo alipaswa kuomba radhi.”Kwa upande wake Werema alimtaka Lissu kufuta kauli yake na kwamba ikiwa hatafanya hivyo basi awasilishe vielelezo vinavyothibitisha madai kwamba majaji huteuliwa bila kufanyiwa uchunguzi.“Lissu ni mtaalamu wa sheria, lakini kauli yake  imewafedhehesha majaji na inashangaza inapotolewa na wakili machachari kama yeye,” alisema Werema.Werema pia alimtaka Lissu kuondoa kauli yake kwa kuwataja watu ambao sio wabunge kwa kunukuu gazeti la Mwanahalisi lililowataja watu watatu kuwa wamehusika na mauaji ya Dk Steven Ulimboka.Werema alisema iwapo Lissu hataondoa maneno yake suala hilo lipelekwe katika Kamati ya Maadili.Kwa upande wake, Chikawe alimwombea radhi Lissu kwa majaji akisema anajua hakutoa kauli ya kuwadhalilisha majaji kwa kukusudia.“Lissu amemtuhumu hadi Rais katika uteuzi wa majaji, hili siyo sahihi, uteuzi wa majaji hupendekezwa na tume maalumu inayohusisha majaji wazoefu ambao ndio wanapendekeza majina kwa Rais,” alisema Chikawe.Baada ya maelezo hayo, Mhagama aliamuru Lissu kuondoa kauli yake hiyo baada ya kutakiwa kufanya hivyo na  Werema wakati akifanya majumuisho ya mjadala wa wizara hiyo.Hata hivyo, Lissu alipopewa nafasi alisema hawezi kuondoa kauli yake kwa kuwa mchakato mzima wa kumtaka afanye hivyo haukufuata Kanuni za Bunge.Lissu alinukuu kanuni ya 63 (1) ambayo inasema: “Bila kuathiri masharti ya Ibara ya 100 ya Katiba yanayolinda na kuhifadhi uhuru wa mawazo na majadiliano katika Bunge, ni marufuku kabisa kusema uongo  bungeni kwa sababu hiyo, mbunge yeyote anapokuwa akisema bungeni ana wajibu wa kuhakikisha kwamba anatoa kauli au maelezo kuhusu jambo au suala ambalo yeye mwenyewe anaamini kuwa ni kweli na siyo jambo la kubuni au la kubabaisha tu”.Lissu aliongeza kuwa, Jaji Werema na Mhagama walivunja Kanuni za Bunge kwa kumtaka kuondoa kauli inayodaiwa kuwa ya uongo kinyume bila kufuata utaratibu.Alipoulizwa kuhusu utekelezaji wa hatua hiyo jana, Mkuu wa Serikali Jaji Fredrick Werema alisema kuwa siyo lazima kwa Watanzania kufahamu hilo.“Nilipozungumza jana (juzi) sikuzungumza na Watanzania bali nilizungumza na Bunge, hivyo siyo lazima Watanzania kufahamu jambo hilo na wala sioni sababu za kwa nini liandikwe magazetini,’’ alisema Jaji Werema.
Source from Mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment